Header Ads

MFANYA BIASHARA DAWA ZA ASILI AFUNGIWA KWA KUUZA DAWA ZINAZOPASWA KUUZWA PHARMACY


Na Fauzia Mussa, Zanzibar

BARAZA la Tiba asili na tiba mbadala Zanzibar, kwa kushirikiana na Wakala wa chakula na Dawa (ZFDA), wamelifungia duka la dawa asili maeneo ya kwa Hajitumbo kutokana na kuwepo kwa  dawa za hospitali katika duka hilo.

Hayo yamebainika kufuatia ukaguzi uliofanywa na baraza hilo katika baadhi ya maduka yaliopo mkoa wa Mjini Magharibi.

Mrajisi wa baraza  la Tiba asili na tiba mbadala Zanzibar,Mohammed Mshenga  Matano akizungumza na waandishi wa habari baada ya ukaguzi huo alisema kufanya hivyo  ni kosa kisheria.

Aidha alieleza kuwa baraza haliridhishwi na tabia ya  wafanyabiashara kama  hao wanaochanganya dawa za asili na  dawa za hospitali kwani mbali ya kwenda kinyume na sheria lakini pia wanahatarisha afya za jamii.

“Katika duka hili tumebaini uwepo wa   dawa zisizostahiki kuuzwa hapa, kwani muuzaji hawezi  kutoa  maelezo sahihi ya kutumia dawa hizi  zinazoelekeza zitumiwe kwa mujibu wa maelekezo ya daktari” Alisema

Alisema uzowefu unaonesha kuwa wafanyabiashara wengi wa  dawa za asili hawana utaalamu wa dawa za hospitali, hivyo endapo dawa hizo zitatolewa bila muongozo wa daktari zitaleta athari kwa mtumiaji.

Mbali na hayo alieleza   kuwa baadhi ya dawa hizo zimemaliza muda wa matumizi na kutoa wito kwa jamii kutumia dawa kwa ushauri na maelekezo ya daktari ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza.

Alizitaja baadhi ya dawa zilizobainika   katika duka hilo  kuwa ni pamoja na  dawa za kuongeza nguvu za kiume, pamoja na za kutibu magonjwa ya wanawake ambazo zote zinahitaji muongozo wa daktari wakati wa kuzitumia.

Alisema licha ya Baraza hilo kuchukua juhudi ya  kuwapatia elimu watoa huduma za tiba mbadala wakati wa  ukaguzi lakini bado baadhi ya wadau hao wanaendesha biashara hiyo kinyume na taratibu zilizowekwa.

Alieleza  Kwa mujibu wa sheria namba nane ya mwaka 2008 ya baraza hilo hatua zinazopaswa kuchukuliwa kwa makosa kama hayo  ni pamoja na  kuziondoa sokoni dawa hizo,au kutozwa faini  isiyopungua laki moja na isiyozidi laki mbili, au kifungo kisichopungua mwezi mmoja na kisichozidi miezi 6, au adhabu ya kusitisha huduma hadi taratibu zitakapokamilika au vyote kwa pamoja.  

Mkuu wa divisheni ya vipodozi walala wa dawa na chakula (ZFDA), Mfamasia Salim Hamad Kassim alisema  wataendelea  kushirikianana na baraza la tiba asili na tiba mbadala ili kuondoa changamoto hizo na  kuleta matokeo chanya kwa jamii.

Alifahamisha kuwa  endapo dawa za hospitali  zitahifadhiwa vibaya au kuingizwa nchini bila utaratibu unaokubalika kutaleta athari moja kwa moja kwa mtumiaji wa miwsho, hivyo ZFDA itashirikiana na kila mdau katika kulinda afya za wananchi.

Hata hivyo alilishukuru baraza hilo kwa ukaguzi wao uliosaidia kuibua maovu ya wadau wa tiba asili dhidi ya jamii, na kuishauri jamii  kuacha kununua na kutumia dawa kiholela ili kulinda afya zao .

Mmiliki wa duka hilo Mwatima Bakari Mussa  alikiri kufanya kosa hilo na kuiomba radhi   Serikali na jamii  kwa ujumla kutokana na makosa hayo  aliyodai kufanywa bila kujua.

Alifahamisha kuwa duka hilo limekua likipokea dawa kutoka sehemu mbalimbali bila kuangalia uhalali na ubora wake, hivyo aliiahidi kuwa makini wakati wa kupokea dawa hizo ili kuepusha  kutokea tena kwa makosa kama hayo  dukani hapo.

Baadhi ya wafanyabiashara  waliokua karibu na duka  hilo waliwashauri wafanyabiashara  wa tiba asili kujali afya za watumiaji na sio kuzingatia maslahi binafsi.

walisema uzowefu unaonesha kuwa jamii haina uelewa juu ya dawa hizo hivyo ipo haja kwa ZFDA na baraza la tiba asili kutoa elimu ili kuwasaidia kulinda afya zao.

Dawa zilizokamatwa 
 

No comments