Header Ads

SERIKALI INAWATEGEMEA VIJANA WABUNIFU

Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula akihutubia wakati akifungua rasmi sherehe za mahafali ya 23 ya Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi za Dar es Salaam, Zanzibar na Tanga yaliyofanyika Desemba 19, 2025, Makao Makuu ya Taasisi hiyo Kurasini Jijini Dar es Salaam
.................................

Na Mwandish Wetu, Dar es Salaam

SERIKALI inawategemea vijana wabunifu, waadilifu na watumiaji mahiri wa teknolojia katika kuleta mabadiliko chanya katika jamii.

Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 23 ya wahitimu wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania Kampasi za Dar es Salaam, Zanzibar na Tanga yaliyofanyika Desemba 19, 2025 Makao Makuu ya Taasisi hiyo Kurasini Jijini Dar es Salaam.

Nimefurahishwa kuona Taasisi ikiendelea kuhimiza ubunifu kupitia mashindano ya mawazo bunifu kwa wanafunzi. Hatua hii inawajengea vijana kujiamini, kufikiri kwa ubunifu na kuwa wazalishaji wa fursa badala ya kuwa watafuta ajira pekee,” alisema Luswetula.

Luswetula aliwaambia wahitimu hao kuwa katika dunia ya sasa, watumie teknolojia, hususan Akili Bandia (AI) na mitandao ya kijamii, kubuni fursa za kiuchumi na kuongeza kipato.

“ Vijana wa leo wanaita hii kuwa “Content Creator” nawasihi muwe content creators wenye tija, mnaozalisha maudhui yenye thamani, yanayoongeza kipato kwa njia halali, kuzingatia maadili na kufuata sheria na taratibu za nchi yetu,” alisema Luswetula na kusisitiza ‘VIJANA NI UBUNIFU, UBUNIFU NI UJANA’.

Aidha Luswetule alitumia nafasi hiyo kutoa shukrani za dhati kwa Afisa Mtendaji Mkuu wa TIA, Profesa William Pallangyo, Menejimenti, Bodi ya Ushauri ya Wizara, watumishi wa Taasisi pamoja na wazazi, walezi na wadau wa elimu, kwa mchango wao mkubwa katika kuwaunga mkono wahitimu na kuimarisha rasilimali watu kwa Taifa.

“ Ndugu Mwenyekiti, Niwapomgeze sana kwa idadi hiyo ya wahitimu 11,382 kwenye kampasi zote tatu. Hii inaonesha ukongwe na weledi katika utoaji wa mafunzo, utafiti, ushauri wa kitaalam,” alisema.

Luswetula aliongeza kuwa kwa kuzingatia muelekeo wa maendeleo na faida za kijiografia, Dar es Salaam, Zanzibar na Tanga ni miongoni mwa maeneo muhimu yanayoendelea kukua kwa kasi na kuwa nguzo ya uchumi wa Taifa.

Alisema Dar es Salaam inaendelea kuwa kitovu cha biashara, bandari na huduma za kifedha; Zanzibar ni lango muhimu la utalii, uchumi wa buluu na biashara ya baharini na Tanga ikiwa na nafasi ya kimkakati kupitia bandari, kilimo cha mazao ya kimkakati, viwanda na utalii wa fukwe hivyo maeneo hayo yanatoa fursa nyingi kwa wahitimu hao  kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi.

Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Taasisi hiyo Profesa William Pallangyo alisema sherehe za Mahafali hayo ya mwaka huu yamejumuisha Kampasi za Dar es Salaam, Zanzibar na Tanga ambapo alitumia nafasi hiyo kutoa pongezi za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuchaguliwa tena kuiongoza Tanzania kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, pamoja na viongozi mbalimbali.

Aidha, Pallangyo alitumia hafla hiyo kuelezea kwa kifupi baadhi ya mafanikio yaliyopatikana na Taasisi ya Uhasibu Tanzania katika utekelezaji wa majukumu yake ya msingi ya kutoa elimu, kufanya tafiti na kuendeleza rasilimali watu wa Taifa.

Alisema Taasisi hiyo ina kampasi katika kanda mbalimbali za Tanzania ambazo ni Dar es Salaam, Singida, Mbeya, Mtwara, Mwanza, Kigoma, Tanga na Zanzibar. Taasisi ina jumla ya wanachuo 40,000. Kati yao, Kampasi za Dar es Salaam, Tanga na Zanzibar zina wanachuo 25,271, sawa na asilimia 63.2, hali inayoonesha mchango mkubwa wa kampasi hizo katika uzalishaji wa rasilimali watu wa Taifa.

Afisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa TIA, Profesa William  Pallangyo akizungumza.
Maandamano ya kitaaluma yakifanyika.
Wahadhiri wakiwa kwenye mahafali hayo.
Wahitimu wakiwa kwenye maandamano hayo.
Muhitimu Hellen Ngete akikabidhiwa cheti pamoja na fedha.
Bras Bnd ya Jeshi la Magereza ikiwajibika katika mahafali hayo.
Wazazi, Ndugu, Jamaa na Marafiki wakiwa kwenye mahafali hayo.
 

No comments