Header Ads

ULEGA, DIWANI KATA YA VIKINDU VIONGOZI WA MFANO, WASIKIVU KWA WANANCHI

Mbunge wa Jimbo la Mkuranga na Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega
...............................................

KIONGOZI wa mfano ni mtu mwenye maono, anayeishi kulingana na maadili anayohubiri, na anayewezesha wengine kufanikiwa.

Kiongozi huyu huongoza kwa vitendo badala ya maelekezo tu, akijenga mazingira ya kuaminiana na kutoa mwelekeo chanya.

Mbunge wa Jimbo la Mkuranga ambaye pia ni Waziri wa Ujenzi, Mhe.Abdallah Hamisi Ulega na Diwani wa Kata ya Vikindu, Mohamed Maundu ni viongozi wa mfano, wanaojali na ni watu wenye upendo, huruma, na wanaothamini uwepo wa watu wengine bila kujali maslahi binafsi.

Mhe. Ulega licha ya kuwa na majukumu mengi ya kitaifa kupitia nafasi yake ya Uwaziri amekuwa mtu wa kujali changamoto mbalimbali za wananchi wake jimboni.

Kwa muda mrefu hasa kipindi cha mvua za masika wakazi  wa Kitongoji cha Mpera kilichopo Kijiji cha Kisemvule Wilaya ya Mkuranga Mkoa wa Pwani walikuwa katika changamoto kubwa kutokana na  kutokuwa na barabara ya uhakika baada ya karavati linalounganisha maeneo hayo kusombwa na maji.

Wananchi hao wameanza kupata matumaini makubwa baada ya mbunge wao kusikikia kiliochao na kuanza kujenga karavati hilo hatua ambayo imewafurahisha.

Hali ya kutokuwepo kwa karavati hilo iliwafanya wananchi hao kutumia gharama kubwa ya usafiri kufuatia eneo hilo kutegemea usafiri wa bodaboda pekee.

Mkazi wa eneo hilo ambaye hakupenda kutaja jina lake akizungumza na Mwandishi wetu, Mei 14, 2026, alisema kukosekana kwa barabara hiyo kumechangiwa na mvua zinazoendelea kunyesha  kusomba karavati la mto Bavu linalounganisha Kijiji cha Kisemvule na kitongoji hicho.

 Hussein Jongo ambaye ni mkazi wa kitongoji hicho, alisema licha ya changamoto ya barabara katika shule za eneo hilo kunaukosefu mkubwa wa miundombinu ya madarasa na  madawati kwani wanafunzi wanakaa chini.

Kwa upande wake Juma Koleza alisema changamoto ya barabara katika eneo hilo ni kubwa ingawa jitihada ndogo ndogo zimekuwa zikifanyika hasa kwenye karavati la mto Bavu.

Alisema eneo hilo limekuwa likijengwa mara kwa mara na mara ya mwisho Mwenyekiti wa Kijiji hicho alifanya jitihada za kukata magogo ya minazi ili yasaidie watu kupita lakini nayo ilisombwa na maji na sasa linatumika daraja la muda la miti ambalo magari hayawezi kupita zaidi ya bodaboda au Toyo.

“Changamoto hii inafahamika hadi Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga kinachosubiriwa mvua ziache kunyesha ndipo waanze ujenzi wa daraja,” alisema Koleza.

Diwani wa Kata ya Vikindu kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mohamedi Maundu akizungumzia kuhusu changamoto hiyo alisema mipango waliyonayo na Mbunge wa Jimbo la Ulega ambaye ni Waziri wa Ujenzi ni kwenda kujenga karavati katika eneo hilo hatua.

“Mpango wetu ni kwenda kujenga karavati katika eneo hilo na tayari tumekwishapata karavati la dharura na ndani ya siku tatu ujenzi wa karavati hilo utakuwa umekamilika,” alisema Maundu.

Ni hatua nzuri iliyofanywa na Mhe. Ulega pamoja na Diwani wa Kata ya Vikindu kwani Mei 16, 2026 siku mbili baada ya mwandishi wetu kuzungumza na wananchi kuhusu kero hiyo walipeleka karavati na kuanza ujenzi mara moja na kudhibitisha kwa vitendo kuwa ni viongozi wa mfano na wasikivu katika kuwatumikia wananchi.

“Mbunge wetu Abdallah Ulega na diwani Maundu hakika wanakwenda na kasi ya utendaji kazi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan,” alisema Hawa Omari mkazi wa kata hiyo.

Diwani waa Kata yaa Vikindu, Mohamed Maundu.
Hali ilivyokuwa kabla ya Karavati kujengwa kwenye eneo hilo ambapo hivi sasa magari ya aina zote yanapita kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na viongozi hao.

...................................

Taarifa hii imeandikwa na Dotto Mwaibale namba ya simu 0754362990.

 

No comments